Bwana YESU atukuzwe ndugu yangu.

Karibu tujifunze Neno la MUNGU  kisha tuombe maombi ya ushindi mkuu.


 Isaya 60:11 '' Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; Hayatafungwa mchana wala usiku; Ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa, Na wafalme wao wakiongozwa pamoja nao.''

Katika ulimwengu wa roho baraka zako zote huwa ziko katika maeneo ambapo ili upate baraka yako uitakayo unatakiwa kubisha kwenye ulimwengu wa roho wa nuru ili ufunguliwe na kuchukua baraka yako, ndio maana katika maombi imani ni jambo la muhimu sana.

Kuna baraka nyingi sana ambazo unazihitaji katika maisha yako.

Kuwa na afya njema ni baraka, kuna na mchumba kisha ndoa ni baraka, kufaulu masomo ni baraka, kuwa na ufahamu mzuri ni baraka, kumiliki nyumba au kiwanja ni baraka, kupata kazi nzuri ni baraka , Kununua gari ni baraka, kupandishwa cheo kazini ni baraka na hata kuwa na uchumi mzuri ni baraka, N.k maana baraka ziko nyingi sana.

Bwana YESU siku moja akatoa siri ya ushindi katika maombi akisema;

‘’Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana BABA yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?   -Mathayo 7:7-11‘’

Kuna kuomba, kuna kutafuta kwa njia ya maombi na kuna kuomba kufunguliwa mlango kwa njia ya maombi,  ndio kubisha huko. 

Kama kuna kubisha basi kuna mlango pia maana huwezi kugonga hodi ukutani na ukuta ukafunguka bali utagonga hodi mlangoni na mlango utafunguliwa.

Baraka  mfano wake ni kama kiti ambacho kipo ndani ya nyumba na wewe uko nje umesimama huku unatamani kukaa maana umechoka kusimama. Kama utataka kukikalia kile kiti ambacho kiko ndani inakubidi kufungua mlango na kuingia ndani na kukichukua kisha unatoka nje na kukiweka chini kiti hicho na unakaa kwa furaha zako.

Nyumba hiyo ni ulimwengu wa roho na kiti ni baraka yako. Sasa ili uchukue kiti na kukikalia inakubidi kwanza uuone malango kisha kama mlangoni kuna adui basi hakikisha unamuondoa adui huyo kwa maombi ya vita kupitia jina la YESU KRISTO. Kisha baada ya kumuondoa adui huyo unafungua mlango kwa maombi kwa imani katika jina la YESU KRISTO. Baada ya kufungua mlango unaingia ndani kwa maombi ya imani kwa jina la YESU KRISTO na unachukua baraka yako na kutoka nje ndipo katika ulimwengu wa mwili itaonekana baraka hiyo na  utaanza kuitumia baraka yako hiyo. Kama ni mume wako ukimfungua kwa maombi katika ulimwengu wa roho ndipo utaona anabadilika katika ulimwengu wa mwili na kuwa mtu mzuri tu bila kukusaliti tena.

Kama umefungua kamba zilizikuwa zimemnasa mchumba wako baada ya maombi utamuona mchumba wako katika ulimwengu wa mwili na utaona akianza mikakati ya posa au mikakati ya ndoa. Ila ni lazima kwanza ushinde katika ulimwengu wa roho ndipo utaona ushindi katika ulimwengu wa mwili.

Ukiona mtu ni Askofu ni kwa sababu alianza kuwa Askofu kwanza katika ulimwengu wa roho ndipo akaja kuwa Askofu katika ulimwengu wa mwili.

Ukimuona mtu ni rais au waziri ni kwa sababu alianza kuwa waziri kwanza katika ulimwengu wa roho ndipo akaja kuwa waziri katika ulimwengu wa mwili.

Ukiona ndoa ina furaha ni kwa sababu kwanza walishinda katika ulimwengu wa roho ndipo wakaja kuona ushindi katika ulimwengu wa mwili.

Kila jambo huanzia kwenye ulimwengu wa roho ndipo linakuja kutokea katika ulimwengu wa mwili.

MUNGU hukujulisha sana kwa njia ya ndoto na maono kile kinachoendelea katika ulimwengu wa roho ili kwa maombi yako kama ni kizuri ukimiliki katika ulimwengu wa mwili na kama ni kibaya ukiharibu katika ulimwengu wa roho ili kisije kutokea katika ulimwengu wa mwili.

Mtu mmoja alikuwa anaota ndoto mara kwa mara akiwaongoza watu wengi na kuwapangia majukumu. Wakati anaota ndoto hizi alikuwa ni maskini wa kutupwa katika familia yao na hakukuwa na uwezekano wa yeye kuja kuwa kiongozi mkubwa katika taifa. Lakini kwa uaminifu kwa MUNGU na kukaa kwenye kusudi lake MUNGU alikuja  kuwa kiongozi mkubwa katika taifa.

Yusufu katika Biblia aliona ndugu zake wakimwinamia na aliona akiwa kiongozi mkubwa na jambo hilo likaja kutokea maana mambo yote huanzia katika ulimwengu wa roho kabla ya kuja kutokea katika ulimwengu wa mwili.

Mwanzo 36:5-11 '' Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili. '' 

Hapo ni mfano mmoja tu katika mifano nyingi ambayo inathibitisha kwa kila jambo linalotokea katika maisha ya mtu limeanzia katika ulimwengu wa roho kabla ya kuja kuonekana katika ulimwengu wa mwili.

Yusufu alianza kuwa kiongozi mkubwa katika ulimwengu wa roho ndipo miaka ya baadae akaja kuja kuwa kiongozi mkubwa yaani akaja kuwa waziri mkuu katika taifa la ugenini na wale ndugu zake waliomwinamia  ndotoni ndio hao hao walikuja kumwinamia katika ulimwengu wa mwili.

Mwanzo 41:38-44 '' Farao akawaambia watumwa wake, Tupate wapi mtu kama huyu, mwenye roho ya MUNGU ndani yake? Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa MUNGU amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake. Akampandisha katika gari lake la pili alilokuwa nalo. Na watu wakapiga kelele mbele yake, Pigeni magoti. Hivyo akamweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akamwambia Yusufu, Mimi ni Farao, na bila amri yako, mtu asiinue mkono wala mguu katika nchi yote ya Misri.''

Miaka mingi baade Yusufu aliwaona ndugu zake na akazikumbuka zile ndoto maana kila jambo huanzia katika ulimwengu wa roho ndipo linakuja kutokea katika ulimwengu wa mwili.

Mwanzo 42:8-9 ''Yusufu akawatambua nduguze, bali wao hawakumtambua yeye. Yusufu akazikumbuka zile ndoto alizowaotea. Akawaambia, Wapelelezi ninyi, mmekuja ili mwuone utupu wa nchi. ''

Kwa Yusufu haikuishia hapo tu kupewa cheo kikubwa katika taifa la ugenini bali hata ndugu zake wale aliowaona katika ndoto zamani na wao walikuja kumwinamia  kama alivyoona katika ndoto zamani(Mwanzo:43:28)

Ndugu yangu naomba ujue kwamba vitu vyote vinavyokutokea katika ulimwengu wa mwili ni kwa sababu vilianza katika ulimwengu wa roho.

Unaweza kutaka kununua kiwanja katika eneo fulani lakini katika ulimwengu wa roho ukaona vita kubwa, unatakiwa umpige kwanza kwa jina la YESU mkuu wa kipepo aliyelishikilia eneo hilo, limiliki kwanza katika ulimwengu wa roho kwa maombi.

Mnaweza kuwa na vita kubwa na mchumba wako kumbe kuna wakuu wa giza wa kiukoo mnatakiwa muwaponde kwanza kwa mawe ya MUNGU.

Unaweza kuwa ni mwimbaji na unataka kurekodi nyimbo zako za injili lakini kabla ya kurekodi unaona vita kubwa kumbe kuna mkuu wa giza ambaye anajua kabisa kwamba kama ukirekodi hakika nyimbo zako zitakuwa chanzo cha watu wengi kuokoka, mharibu kwanza kizuizi huyo wa kipepo, mharibu kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Kama mtu anaumwa maana yake alianza kuumwa kwanza katika ulimwengu wa roho ndipo akaja kuumwa katika ulimwengu wa mwili, kama ukiudhibiti ugonjwa kwa maombi katika ulimwengu wa roho hakika ugonjwa huo hutauona katika ulimwengu wa mwili.

Tatizo lako ukilishinda katika ulimwengu wa roho hakika na kwenye ulimwengu wa mwili utalishinda jambo hilo.

Ndugu mmoja alikuwa anaota ndoto mara kwa mara anabadilika na kuwa wanyama mara wadudu mara ndege za ajabu ajabu na kupaa.

Siku moja akaota anakuwa ngome na kutembea, siku nyingine akaota akiwa binadamu kama kawaida ila   ana mapembe kama ya ng'ombe, Siku nyingine akaniambia ameota anatembea ghafla akageuka na kuwa bundi na kuweza kuruka.
Nilimwambia kwamba roho ya uchawi inamfuatilia au inamtumia kabisa bila yeye kujua. 

Kuna watu hutumika kichawi bila wao kujua.

Watu wa rohoni wanaweza wakajua kabisa kwamba wewe ni mchawi kwa sababu wanakuona katika ulimwengu wa roho na huku wewe mwenyewe wala hujui kama ni mchawi maana hujawahi kumroga mtu, lakini kumbe unatumika kichawi bila kujua. Huyu baada ya miezi kadhaa akaniambia kwamba wanataka kumfanya kuwa kiongozi wa ukoo wao na kwa jinsi hiyo ametakiwa kujifunza madawa na uchawi kidogo. Nikamkumbusha kuhusu ndoto zile na hatari zake.

Ndugu zangu adui akikuweza katika ulimwengu wa roho hakika na katika ulimwengu wa mwili atakuweza pia ndio maana huwa unaona mipango ya shetani juu yako kupitia ndoto ili tu uombe kinyume na mipango ile na haitakutokea.

Unaweza ukaota umekufa na kwa sababu huoni ukifa ukadharau kumbe hakika unakuja kufa kiroho au uchumi wako unakufa au kazi yako inakufa. Kila jambo huanzia katika ulimwengu wa roho ndipo linakuja kutokea katika ulimwengu wa mwili.

Unaweza kutaka kufungua biashara fulani katika eneo fulani, pesa unayo ya kutosha kabisa lakini unaona ugumu sana juu ya jambo hilo, unatakiwa umharibu kwanza kizuizi wa kipepo aliyelishikilia eneo hilo.

Nimeanzia mbali ili unielewa vizuri zaidi katika somo la leo la kumiliki milango ya baraka aliyokuwa ameishikilia adui.

 Kwa sababu umenielewa juu ya vitu vyote kuanzia katika katika ulimwengu wa roho twende sasa kwenye kiini cha somo langu na maombi.

Mwanzo 22:17 ‘’ katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao;‘’

Uzao wa Ibarahimu ulipewa kibali na MUNGU cha kumiliki milango ya baraka ambayo adui alikuwa ameikalia.

Uzao wa Ibrahimu ni wateule wote wa KRISTO waliookoka.

mimi Peter Mabula na wewe ndugu uliyeokoka ni uzao wa Ibrahimu na warithi sawasawa na ahadi ya MUNGU.

Wagalatia 3:29 ''Na kama ninyi ni wa KRISTO, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.''

Kuna siri kubwa katika Neno Kumiliki milango ya adui.

Kama unavyoona kuna utawala wa kiserikali katika kila eneo ndivyo hivyo hivyo shetani naye na jeshi lake anao utawala katika kila Eneo. 

Ndio maana Biblia inawataja watawala wa kishetani ikisema;

 ''Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.-Waefeso 6:12''

Unalishawahi kujiuliza kwamba hao maadui zetu ambao ni falme za kipepo, mamlaka za kishetani, wakuu wa giza na majeshi ya pepo wabaya huwa wako wapi?

 Ni serikali ya kishetani inayotawala ambayo wewe mteule wa KRISTO una mamlaka kuliko hiyo serikali  ila tu kama utaitumia hiyo mamlaka yako ya KRISTO kwa maombi.

Kama ambavyo unapohamia mtaa fulani au kijini fulani utaripoti kwa viongozi wa kijiji au mtaa ndivyo hivyo hivyo ulimwengu wa roho wa giza una viongozi wa kipepo katika kila Eneo hivyo ili ulikamate eneo hilo ni lazima uwashinde viongozi hao wa kipepo.

Inawezekana hujanielewa lakini ngoja nitoe mifano;

Askofu Moses Kulola kabla ya kuanza kuhubiri injili ya mafanikio makubwa katika Tanzania aliingia katika maombi ya kufunga siku 4 mlimani. Katika maombi hayo akiwa katika siku ya mwisho ya maombi aliona jitu kubwa la kutisha likija alipo na lilipokaribia lilimwambia kwanini anataka kulichukua eneo lake huyo mkuu wa giza, yaani Tanganyika kwenye ulimwengu wa roho wa giza kulikuwa na mtawala wake ambaye ndiyo huyo roho ya kuzimu, kwa maombi Askofu Moses Kulola alimshinda yule mtoto wa shetani ndio maana akaanza kuhubiri injili ya mafanikio sana. Kila Eneo huwa lina utawala wa aina tatu. Kuna utawala wa kibinadamu, kuna utawala kutoka ulimwengu wa roho wa giza na utawala wa MUNGU hutawala pote na una mamlaka ya mwisho.

Kumbe ili ulipate eneo fulani kwa ajili ya kitu fulani chako chema inabidi kwa maombi umpige mkuu wa giza wa eneo husika.

Biblia inasema wateule watakapopakanyaka patakuwa pao maana yake watakuwa na mamlaka ya kupatiisha kwa jina la YESU waliyenaye, hata utawala wa shetani utasalimu amri maana wao wana Bwana YESU mwenye nguvu zote milele.

David Yonggi Cho wa Korea kusini Ni mhubiri mwenye kanisa kubwa wanaloabudu pamoja kuliko makanisa yote duniani. Alipoitwa na Bwana YESU ili amtumikie alianza kumtumikia. Lakini mwanzo tu wa huduma yake aliona mkuu wa giza anayelimiki eneo la Korea yote. Ilibidi  Mchungaji Yonggi Cho apambane kwa maombi na mkuu yule giza. alipomshinda kwa maombi kupitia jina la YESU ndipo huduma yake ilistawi na huduma hiyo imefikia hatua ya sadaka zinahesabiwa kwa zaidi ya siku 2 na sadaka hiyo kuipeleka bank ni kwa msafara mkubwa kukiwa na ulinzi mkubwa wa Polisi wengi.

Ndugu, ukishinda katika ulimwengu wa roho hata katika ulimwengu wa mwili utashinda pia.

Leo omba ukimtoa aliyekaa katika mlango wa baraka yako katika ulimwengu wa roho.

Omba ukifungua mlango wa baraka yako na kwa imani chukua baraka yako ili ije ionekane katika ulimwengu wa mwili.

Bwana YESU amekufungulia mlango wa baraka mbele yako. Ni kazi yako tu kupambana kwa njia ya maombi ili upate baraka zako ambazo utazipata ndani baada ya kuingia kupitia mlango huo.

Ufunuo 3:8 ''Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.''

Mwanzo kabisa Isaya 60:11 inasema kwamba malango yako au milango yako itakuwa wazi lakini haiwi wazi bila wewe kuomba iwe wazi.

Baraka zilizoahidiwa katika andiko hilo hazitakuja kwako bila maombi na utakatifu katika KRISTO.

Leo Ondoa maadui waliokaa katika milango yako ya baraka .

Fungua milango ya baraka zako.

chukua baraka yako.

Baada ya kuomba maombi ya toba ya kweli na kuacha uovu nakuomba omba maombi haya chini kama wewe ni muombaji mchanga lakini kama wewe unajua kuomba basi huhitaji maombi haya ila kwa sababu umelielewa fundisho basi omba ukiliiendea hitaji lako.
Ukipata msukumo wa kunisapoti huduma yangu kwa sadaka ya hiari fanya hivyo pia maana kuna ratiba za kuchapisha vitabu zaidi, vifaa bora vya kuhubiria n.k
Kazi yangu Mimi ni kukuombea na najua baraka zilizo ndani ya utoaji hazitakupita. 

MAOMBI YA KUMILIKI MILANGO YA BARAKA ALIKUWA AMEISHIKILIA ADUI.

 BABA katika jina la YESU KRISTO aliye hai.
Ninakushukuru na kukuabudu pekee uliye MUNGU muumba mbingu na dunia.
Asante kwa siku ya leo na asante kwa uzima ulionipa katika mwanao YESU KRISTO Mwokozi wangu.

Nakushukuru kwa ufunuo huu wa leo na naomba kwa damu ya YESU na kwa jina la YESU unipe ushindi.

Umesema katika Neno lako katika Mathayo 16:19 Kwamba ''Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni. '' 

Leo nawafunga maadui zako wote walioshikilia milango yangu ya baraka katika ulimwengu wa roho, nawafunga kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Nawatupa kuzimu maadui wote walioshirikia milango ya baraka yangu.

Adui aliyeshikilia mlango wangu wa kupata baraka ya mchumba namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Adui aliyelishikilia eneo langu la biashara hata sipati faida niitakayo, namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Adui aliyeshikilia uchumi wangu,
namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Adui aliyeishikilia ndoa yangu hata inakuwa na migogoro kila siku,namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Adui aliyeishikilia kazi yangu, namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Adui aliyeshikilia kipato changu na kuniletea madeni yasiyoisha,
namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

 Adui aliyeshikilia ufahamu wangu,
namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Adui aliyewashikilia ndugu zangu na ukoo wangu,
namharibu na kumwangamiza adui huyo kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.
Adui jini, roho za kichawi, wakuu wa giza, wakuu wa anga, mizimu,  madhabahu za giza  na kila maroho wa kuzimu, hao maadui nawaharibu na kuwangamiza  kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Kila mlango wa baraka yangu uliokuwa umefungwa sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa kufunga ndoa ndoa ulikuwa umefunga,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa kupata kazi uliokuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa biashara ulikuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa kupanda cheo uliokuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa amani na furaha katika ndoa yangu, sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa huduma na kumtumikia MUNGU uliokuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa kupona magonjwa ulikuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa furaha katika familia uliokuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Mlango wa mafanikio ya rohoni na mwilini uliokuwa umefungwa,sasa naufungua kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO.

Kila mlango wa baraka yangu ulikuwa umefungwa  leo naufungua kwa jina la YESU KRISTO aliye hai.

Sasa naita baraka yangu iliyo katika ulimwengu wa roho ili ije sasa katika ulimwengu wa mwili.

Namuita mchumba wangu aliyekuwa amezuiliwa katika ulimwengu wa roho, Namwita kwa jina la YESU KRISTO aliye hai. Ewe Mchumba njoooooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ninaiita kazi yangu kwa jina la YESU KRISTO.

Ewe kazi yangu njoooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ewe uzima njoooooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ewe ufahamu mzuri darasani njooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ewe ndoa safi njoooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ewe Kiwanja njooooooooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ewe nyumba njooooooooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Naita furaha na amani Katika ndoa yangu,  Ewe furaha na amani njooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Naita uzao,  Enyi watoto wa kiume na wa kike  njooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.
Ewe huduma nzuri njooooooooooo kwa jina la YESU KRISTO.

Ninaita baraka zangu zote kwa jina la YESU KRISTO zije.

Kwa jina la YESU KRISTO kila mlango wa baraka yangu utakuwa wazi kama Isaya 60:11 inavyoseama na hakuna adui hata mmoja atakaye ufunga mlango wa baraka yangu.

Nazifunika kwa damu ya YESU KRISTO baraka zangu zote na adui hatazipata kamwe.

Nakushukuru JEHOVAH MUNGU wangu kwa ushindi wa ajabu ulionipa leo.

Jina lako litukuzwe MUNGU uliye hai.

Katika jina la YESU KRISTO Mfalme wa uzima na ushindi, nimeomba na kupokea ushindi.

Amen Amen.

Ndugu uliyesoma ujumbe huu ubarikiwe sana.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu. 
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa BWANA YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.
+255714252292.

Ukishare somo hili Kwa maandishi nakuomba sana ulifute majina na  chochote kile kilicho ndani ya somo hili.
Axact

Tanzania Worships

Haleluyah! Karibu katika ukurasa wa Tanzania Worships ambao ni maalumu kwa ajili ya kusambaza na kulihubiri Neno la Mungu anayeishi. je kuna maoni na ushauri unataka kuuutoa ili kuhakikisha ukurasa huu unawafikia waamini na wasioamini? basi usione shaka kuwasiliana nasi kwa njia ya mitandao ya kijamii

Post A Comment:

0 comments: